
“Maana mwaijua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba alikuwa maskini kwa ajili yenu, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.”
2 Wakorintho 8:9
Wakristo wengi humtafuta Mungu kana kwamba bado wanajaribu kumshawishi awabariki. na wakati Neno la Mungu linatufundisha tofauti kabisa, kwamba kupitia kazi ya Yesu Kristo msalabani, tayari tumepokea urithi mkuu ndani yake (Utajiri). Yesu alijitoa kwa ajili yetu ili tuingie katika utajiri wa neema yake na urithi wa ahadi zote ambazo Baba ameweka kwa watoto wake.
Hii inamaanisha kuwa kabla hatujaona matokeo katika ulimwengu wa mwili, Mungu tayari ameweka ndani yetu uwezo, neema, hekima, vipawa na ahadi zinazohitajika ili tuishi maisha yenye ushindi na utajiri. Na ili Kile kilichopo katika ulimwengu wa roho kiweze kudhihirishwa katika maisha yetu ya kila siku, basi hatuna budi ila kutembea katika utii kwa Roho Mtakatifu na kufanya kazi kwa bidii.
Roho Mtakatifu hutuelekeza kupitia Neno la Mungu. Mara nyingi maelekezo yake yanahusisha kufanya kazi kwa bidii, kutumia vipawa vyetu kwa uaminifu, kuwa waadilifu, kujifunza, kuhudumia wengine kwa ubora, na kusimamia vizuri kile ambacho Mungu ametukabidhi. na kila wakati tunapotii maelekezo hayo kwa imani, tunafungua nafasi ya kuona kile ambacho Mungu ameweka ndani yetu kikionekana katika maisha yetu.
Ndiyo maana ni muhimu kuwa na mtazamo wa kiimani kuhusu utajiri. Mtu anayeamini kwamba Mungu amemwandalia urithi wa baraka hufanya maamuzi tofauti katika mambo ya kila siku ukilinganisha na yule asiye amini. Hataongozwa na hofu au mawazo ya upungufu, bali atatafuta maarifa, atafanya kazi kwa bidii, atatumia muda wake kwa hekima, atawekeza katika ukuaji wake, na atatafuta fursa ambazo Mungu anafungua mbele yake. Imani hubadilisha jinsi tunavyofikiri, na jinsi tunavyofikiri huathiri maamuzi tunayofanya kila siku.
Usikubali kuishi kwa mtazamo wa umaskini wakati Mungu amekuita kutembea katika utajiri wa neema yake. Amini kile ambacho Mungu amesema kuhusu wewe, fuata maelekezo ya Roho Mtakatifu kupitia Neno lake, na fanya kazi kwa bidii na uaminifu. Kadiri unavyotembea katika maelekezo ya Roho mtakatifu na kufanya kazi kwa bidii ndivyo utakavyoona urithi ambao Mungu ameweka ndani ya Kristo ukizidi kudhihirika katika maisha yako. Barikiwa.








