
“Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa upendo.”
Wagalatia 5:6
Katika kila jambo kuna utaratibu wa namna mambo yanavyo paswa kufanyika ili kutoa matokeo yanayokusudiwa. Na kama ilivyo katika ulimwengu wa mwili vivyo hivyo katika ulimwengu wa roho kuna utaratibu wa namna mambo yanafanyika.
Mungu wetu ameweka ahadi kubwa mno za thamani kwa kila mtu, ahadi hizi zinalenga kutuwezesha kuishi maisha ya usalama, furaha, afya na mafanikio tele. Lakini ili tuweze kuzipata hizo ahadi ni lazima kutumia Imani. Na ili Imani ifanye kazi ni lazima kuwepo na UPENDO. Ndio maan andiko la utangulizi
likasema “…….bali imani itendayo kazi kwa upendo.”
Ndugu mpendwa Upendo kwa Imani ni kama Mafuta katika gari, pasipo upendo Imani haitofanya kazi. Na kama Imani haitofanya kazi basi hauwezi kupokea ahadi za Mungu kwako. Kwa hiyo kama unataka kufurahia yale mengi ambayo Mungu ameweka kwa ajili yako basi hauna budi bali kuenenda katika Imani na upendo kwa watu wote. Barikiwa.








